Makala Na Fatma M. Suleiman
Mitazamo kuhusu nafasi ya mwanamke katika uongozi imeendelea kubadilika taratibu. Wapo wanaoamini kwamba mila na desturi haziruhusu mwanamke kuwa kiongozi, wengine wanaona hakuna pingamizi la kimaadili wala kidini linalozuia mwanamke kushika nafasi za juu za maamuzi.
Bikame Sheha Ussi, Mkuu wa Divisheni ya Pensheni Jamii na Maendeleo ya Wazee, anabainisha kuwa historia za dini pia zinaonyesha wazi kwamba wanawake hawajazuiwa kuwa viongozi.
“Kwa upande wa Dini ya kiislamu haijakataza mwanamke kuwa kiongozi, bali inasisitiza kuzingatia mipaka na maadili.”
Anaongeza kuwa, mfano wa Bi Khadija (R.A.), mke wa Mtume Muhammad (s.a.w.), ni kielelezo cha mwanamke aliyekuwa kiongozi wa kiuchumi na kijamii katika zama zake.
Ni Dhahiri, uwezo wa mwanamke kuhudumia familia na mifano ya wanawake walioleta mabadiliko katika jamii kitaifa na kimataifa ni chachu ya kubomoa mitazamo hasi na mawazo mgando hususan katika zama hizi.
Mkurugenzi wa Ustawi wa Jamii na Wazee Hassan Ibrahim Suleiman anafafanua kuwa, wanawake wana uwezo mkubwa wa kuwa viongozi katika ngazi mbalimbali kuanzia familia, jamii hadi taifa endapo watapatiwa fursa sawa za elimu na uwezeshaji.
Hata hivyo, amebainisha kuwa masharti ya ndoa ambapo baadhi ya waume huwazuia wake zao kushiriki katika shughuli za kijamii na kisiasa, ukosefu wa kipato cha kutosha unaosababisha utegemezi, na rushwa ya ngono, ni vikwazo vinavyowakwamisha wanawake wengi kufikia ndoto za kupata nafasi za uongozi.
Anasema, licha ya jitihada za serikali na taasisi binafsi, kuwekeza zaidi katika elimu ya wavulana kuliko wasichana, kwa dhana kwamba wanaume ndio tegemeo la familia. Anasisitiza kuwa uongozi ni mchakato unaohitaji harakati, muda na dhamira thabiti ambavyo kwa wanawake bado ni mwiba uliowasakama kutokana na majukumu ya kifamilia, mifumo dume na mitazamo hasi.
Wataalam wa maswala ya kijamii wanaamini kuwa elimu ni chachu ya ujasiri, msimamo thabiti, na uwezo wa kufanya maamuzi sahihi katika nafasi za uongozi. Hivyo, Mwanamke aliyeelimika huondokana na vizuizi vya fikra finyu na huchukua nafasi yake kama mshiriki kamili katika maendeleo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi.
Kama anavyobainisha Kafui Adjamagbo-Johnson (2019, UN Africa Renewal) kwamba “Ukosefu wa wanawake kupata elimu bora, maarifa na rasilimali umekuwa kikwazo kinachowazuia kushika nafasi za uongozi barani Afrika.”
Katika kuimarisha mazingira rafiki ya kumwezesha mwanamke kufikia ndoto zake, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeendelea kuimarisha usawa wa kijinsia katika elimu na kuhakikisha sera na mikakati iliyopo inawanufaisha wanawake kufikia safari ya uongozi na 50/50.
Tafiti kutoka Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake TAMWA-ZNZ zinabainisha kuwa tokea mwaka 2024 hadi 2025 imewawezesha takribani wanawake 11,600 na kujengea uelewa kwa masuala ya maamuzi na uongozi .
Ripoti ya Taasisi ya Utafiti wa Masuala ya Jinsia, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM-IGS) 2021, ilionesha kwamba elimu ya uongozi imekuwa chachu muhimu ya wanawake Zanzibar kujiamini na kuwania nafasi za kisiasa.
Nunu Issa Juma, Makamu Mstaafu wa Rais wa Chuo Kikuu cha Zanzibar (ZU), anaeleza kwamba elimu ina mchango mkubwa katika kumjengea mwanamke kujiamini. Amesema:
“Kupitia elimu, nimepata ujasiri mkubwa wa kujieleza na kusimamia hoja zenye msingi.”
Anafafanua kuwa elimu humsaidia mwanamke kutetea haki na kushiriki katika mijadala ya kijamii na kitaifa kwa ufasaha zaidi. Elimu humwezesha kuelewa sheria na misingi ya haki za binadamu, hivyo kuweza kumlinda mwanamke dhidi ya kudhulumiwa.
Aidha, anasisitiza kuwa mafanikio ya mwanamke katika uongozi hayaji kwa bahati, bali kwa kujituma na kuwa na nia thabiti. “Wanawake wanaweza kuwa viongozi bora endapo jamii itabadilisha mtazamo kwamba mwanamke anaweza kuongoza.”amesema Nunu.
Programu za kuwaandaa wanawake kuwa viongozi wa baadae katika vyuo vikuu ikiwemo Chuo Kikuu cha Zanzibar (ZU) kupitia Dawati la Jinsia ni chachu ya inayowaelimisha pia kutambua haki zao na kujiamini katika kuchukua nafasi za uongozi.
Aidha, mchango Chuo kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kwa kushirikiana na TAMWA-ZNZ wamesaidia sana kukuza usawa wa kijinsia kuptia programu za uongozi kwa wanawake
Kila jamii inayothamini maendeleo huanza na uwekezaji katika elimu, humpa mwanamke uwezo wa kushinda vikwazo vya mila, desturi, na mitazamo duni inayomfanya aonekane asiye na uwezo wa kuongoza.
Kwa kuzingatia nafasi kubwa ya elimu katika kubadilisha jamii, Aliyekuwa Raisi wa Afrika Kusini, marehemu Nelson Mandela (1994), amesema “Elimu ni silaha yenye nguvu zaidi ambayo unaweza kutumia kubadilisha ulimwengu.”
Elimu ni nguzo muhimu inayompa mwanamke ujasiri, uelewa, na uwezo wa kushiriki kikamilifu katika uongozi. Hata hivyo, elimu pekee haitoshi bila kujitambua na kuwa na maadili.
“Elimu pekee bila kujitambua haitoshi, uongozi unahitaji msimamo, maadili, na uthubutu wa kweli.”amesema Bikame.
Ili kufikia usawa wa kweli katika uongozi, jamii inapaswa kuendelea kuwekeza katika elimu ya wanawake, kuondoa vikwazo vya kijamii, na kukuza mitazamo chanya kuhusu uwezo wa mwanamke katika uongozi. Elimu ni msingi wa mabadiliko na daraja la kumuinua mwanamke kuwa kiongozi wa leo na wa kesho.
MWISHO

Comments
Post a Comment