NA, HASSAN MSELLEM, PEMBA
KATIBA ZA VYAMA
Katiba za vyama vingi vya Siasa nchini zimezingatia usawa wa Kijinsia katika Uongozi ndani na nje ili kuwepo kwa usawa katika vyama hivyo. Katiba ya Chama cha Mapinduzi CCM, Sura ya Pili Fungu la Pili ibara ya 16 inasema “Kiongozi wa CCM ni kila Mwanachama mwenye dhamana yoyote katika CCM aliyechaguliwa au kuteuliwa kwa mujibu wa Katiba. Ibara ya 17 inaeleza sifa za kiongozi ni pamoja na kutosheka na asiwe mtu aliyetawaliwa na tamaa.
Katiba ya Chama cha Alliance for Change and Transparency - ACT Wazalendo SEHEMU YA PILI, imeeleza Sifa za kuwa kiongozi katika Chama hicho ikiwemo “kuwa na mwenendo mzuri na Maadili ya Viongozi” Lakini licha ya haki ya Usawa wa Kijinsia iliyotolewa na Katiba za vyama Siasa bado Wanawake wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa fedha kuanzia fedha za kuchulia fomu pamoja na kampeni, hali inayosababisha Wanawake wengi kushindwa njia kugombea nafasi za Uongozi kupitia vyama vyao.
WANAWAKE WALIOWAHI KUGOMBEA
Mgombea wa nafasi ya Ubunge kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi Mwamize Mohammed, amesema bado wanawake wanakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwe ukosefu wa fedha, ubaguzi wa kijinsia pamoja na rushwa ya ngono hali inayosababisha wanawake wengi kukosa fursa za kuwa viongozi.
Asema “Bado wanawake tunakabiliwa na changamoto lukuki katika kugombea nafasi za Uongozi kwasababu kama huna fedha za kuwapa wajumbe kwa sera tupu za maneno huwezi kuzingatiwa, kuna changamoto ya rushwa ya ngono binafsi nimekumbana nayo ila nimefanikiwa kuikwepa lakini pia kudharaulika chakusikitisha zaidi wanawake wenzetu ndio vinara wa kuwashawishi wanachama wasituchague”
Mgombea wa nafasi ya Uwakilishi kwa tiketi ya Chama cha ACT Wazalendo katika Jimbo la Wawi Hadija Anuwar Mohammed, amesema licha ya Chama hicho kuwa na Sera ya Usawa wa Kijinsia lakini bado Wanawake wamekuwa wakikabiliwa na khofu ya kugombea nafasi za Uongozi kutokana na dhana potofu kuwa mwanamke hawezi kuwa na uwezo wa kufanya vizuri katika nafasi za uongozi
“Tatizo sio muamko wala kujiamini lakini tatizo wanaume wakikusikia tu kuwa unataka kugombea nafasi ya Jimbo wanakufata na kukushawishi na kukutia khofu kwamba kwanini usigombania nafasi za UWT sasa hiyo ndio inatufanya wanawake kuwa na khofu ya kugombania nafasi za Jimbo ila kwakweli wanawake tuna uwezo mzuri kuliko hao wanaume” Maoni ya Mgombea wa nafasi ya Uwakilishi kwa tiketi ya Chama cha ACT Wazalendo katika Jimbo la Wawi Hadija Anuwar Mohammed
WADAU WA USAWA WA KIJINSIA
Wadau na watetezi wa Usawa kijinsia walisema tatizo la ukosefu wa fedha za kampeni na umashuhuri ni miongoni mwa vikwazo vikuu vinavyowafanya wanawake washindwe kutimiza ndoto zao za kuwa viongozi na badala yake ni wanawake wachache tu wanaohimili mchakato huo.
“Sasa hivi wanawake wameamka sana tukilinganisha na miaka ya nyuma na hii inatokana na elimu na hamasa ambazo tumekuwa tukizitoa kwa muda mrefu Imani yetu Imani yetu ile Sera ya 50 kwa 50 itafanikiwa ifikapo 2030 endapo changamoto zinazowakabili zikipatiwa ufumbuzi” Omar Saleh Mwanamme wa Mabadiliko kutoka Shehia ya Kilindi
JUMUIYA ZA UTETEZI WA HAKI ZA WANAWAKE
Mratibu wa Jumuiya ya Utetezi wa Kijinsi na Mazingira Pemba (PEGAO) Dina Juma Makota, amesema licha ya wanawake wengi kuhamasika kujiunga na vyama vya siasa na kugombea nafasi za uongozi lakini bado wanakabiliwa na changamoto za ukosefu wa fedha, mfume dume na rushwa ya ngono hali inayochangia kuzima ndoto zao.
“Niwaombe wanawake wote wanaopitia changamoto za ubaguzi, unyanyasaji na kudaiwa rushwa ya ngono na fedha kujiamini na kuziripoti changamoto hizo kwa vyombo husika au kwa wadau wa utetezi wa haki za wanawake ili zipatiwe ufumbuzi na sio kuzikalia kimya lakini pia viongozi wa vyama wanatakiwa kubadilika na kuwaamini wanawake kuwa ni viongozi wazuri, mfano mzuri ni Rais Samia kumteua Dkt. Asha Rose Migiro kuwa Katibu Mkuu wa CCM na Waziri wa Ulinzi Mhe. Stagomena Tax na wanafanya vizuri” Mratibu wa Jumuiya ya Utetezi wa Kijinsi na Mazingira Pemba (PEGAO) Dina Juma Makota.
Kaimu Mratibu wa Tamwa Pemba Amina Ahmed, amesema katika kuwasaidia Wanawake wanaokabiliwa na changamoto kipindi cha kampeni na uchaguzi ni kuanzisha Mtandao wa kutoa za Taarifa Za Mapema (Early Worning Network) ili waweze kutoa taarifa za changamoto zinazojitokeza dhidi yao.
“Ssi tukiwa taasisi tunayopaza sauti za wanawake tunazipokea changamoto zote zinazowakabili wanawake wakati huu wa kampeni na kabla ya Uchaguzi tumeanzisha mtandano wa Mfumo wa Taarifa za Awali (Early Worning Network) mtandao unawapa fursa wanawake kupaza sauti zao dhidi ya viashiria vyote vinavyoweza kuwarudisha nyuma katika mchakato wa kugombea, kampeni na kipindi cha Uchaguzi” amefafanua
VIONGOZI WA VYAMA VYA SIASA
Makamo Mwenyekiti Mkutano Mkuu Taifa na Mjumbe wa Halmashauri Kuu Mkunga Hamad Sadala, alisema chama cha ACT Wazalendo ni Chama cha kwanza kuanzisha Sera jinsia lengo likiwa ni kuweka usawa katika chama hicho pamoja na kutambua uwezo na nguvu ya wanawake katika ujenzi wa Taifa.
Aidha Mwenyekiti huyo alisema mkakati wa chama cha ACT Wazalendo ni kuwachukulia hatua kali Viongozi na wagombea watakaobainika kutenda vitendo vya ubadhirifu ikiwemo rushwa ataondolewa katika nafasi anayogombea ili iwe fundisho kwake na wagombea wengine.
“Miongoni mwa mikakati yetu Chama cha ACT Wazalendo katika kudhibiti vitendo vya ubadhirifu ikiwemo rushwa, ubaguzi na kadhalika ni kwamba mgombea yeyote atakaebainika kutenda makosa hayo hata kama ameshinda kwa kura zote hatokuwa tena mgombea wa nafasi hiyo hii itakuwa funzo kwake na kwa wagombea wengine” alisema
Mariam Mohammed Muhene Kamshna Kanda ya Pemba Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC) amesema Chama cha ADC kinazingatia usawa wa Kijinsia na watu wenye mahitaji maalum katika ngazi zote za Uongozi bila ya kuangalia jinsia, rangi wala hali ya mwanachama hali inayochangia idadi kubwa ya viongozi Wanawake katika Chama hicho.
Amesema “Chama chetu ndio chama pekee ambacho kinazingatia jinsia lakini sio jinsia tu bali makundi ya watu wenye mahitaji maalum na hili linadhihirika kwa mifano mbali mbali kwa mfano Naibu Katibu Mkuu wa Chama ni Mwanamke na Makamo mwenyekiti pia ni mwanake lakini katika Baraza Kuu la Uongozi ni 50 kwa 50 hii yote inamaanisha kuwa Chama cha ADC ni chama kinachozingatia zaidi usawa wa Kijinsia kwahivyo katika chama chetu hakuna masuala ya kuwanyanyasa wanawake kwasababu nalisimiamia vizuri hilo ila tu changamoto inayotukabili ni ukosefu wa fedha kwasabau hatuna ruzuku”
Mwisho.

Comments
Post a Comment