Mchezo wa kuogelea ni miongoni mwa michezo maarufu duniani, ingawa kuna idadi ndogo ya wanawake Barani Afrika wanaoshiriki katika mchezo huo ikilinganishwa na wanawake wa Bara Ulaya.
Zanzibar ni miongoni mwa
maeneo yenye idadi ndogo sana ya wanawake wanaoshiriki mchezo wa kuogelea licha
ya Visiwa hivyo kuzungukwa na Bahari, huku na sababu kadhaa zinazosababisha
idadi ya wanawake wanaoshiriki mchezo huo kuwa ndogo.
Miongoni mwa sababu hizo pamoja
na wanawake wenyewe kutokuwa na hamu na shauku ya kushiriki mchezo huo,Mila,
Utamaduni pamoja na Imani potofu kwa baadhi ya wanajamii wakiamini kuwa mchezo
huo ni mchezo unaowahusu wanaume pekee.
Mwezi March, 2022 katika
shamrashamra za kumpokea Rais wa Shirikisho la Mchezo
wa Kuogelea Duniani (FINA) Husain Al Musallam, kutembelea Zanzibar,
Kamishna wa Idara ya Michezo Zanzibar Ameir Mohammed Makame, alisema Sera ya
Michezo Zanzibar yam waka 2018 inasema kuendeleza michezo ya kuogelea ikiwa ni
miongoni mwa michezo 41 iliyosajiliwa Zanzibar.
Balozi wa heshima wa
Brazil Zanzibar, Abdulsamad Abdulrahim alisema ziara ya ais wa Shirikisho la
Mchezo wa Kuogelea Duniani inafanyika ikiwa Zanzibar inajipanga kujenga bwawa
kubwa la kuogelea lenye hadhi ya Olimpiki ambalo linakadiriwa kugharimu dola za
kimarekani milioni 3 sawa na shilingi bilioni 6 na milioni 900, ambalo
litawawezesha vijana wanaoshiriki mchezo wa kuogelea kuwa nae neo mahsusi la
kuogelea tofauti na ilivyo sasa ambapo hushiriki mchezo huo kupitia habarini
kama kawaida.
Lakini licha ya idadi hiyo
ndogo ya wanawake wanaoshiriki mchezo wa kuogelea wapo wanawake ambao wana
vipaji vya kuogelea na kuupenda mchezo huo kiasi ya kuuota usingizini.
Wanawake wa Mji wa Tumbe
Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba, wao wameamua wanawake wa mfano
kupitia mchezo wa kuogelea hasa pale walipogundua kuwa licha ya kutumia mchezo
huo katika mashindano na kujiokoa inapotokea dharura lakini pia ni kwa ajili ya
harakati zao za Maisha ya kilimo cha Mwani na fursa ya kujipatia kipato.
Kaije Said Bakar, ni nguli
na kinara wa mchezo wa kuogelea ambaye ni mwalimu wa wanawake na wasichana
zaidi ya 300 kutoka maeneo tofauti ya Kisiwa cha Pemba, alisema mchezo wa
kuogelea umeweza kumnufisha kwa kiasi kikubwa kama vile kujenga nyumba ya
kuishi na familia yake, kuwalipa ada za masomo Watoto wake pamoja kumsadia
mumewe mkate wa kila siku.
“kwakweli mchezo wa
kuogelea umenisaidia sana sana tena sana maana kabla kujua mchezo huo Maisha
yetu yalikuwa magumu mno tulikuwa tunaishi kwenye banda tu hivi kama hema la
wakimbizi lakini sasa nimejenga nyumba mzuri si haba tumeshajistiri, nawalipia
Watoto wangu ada za Skuli pamoja kumsaidia mume wangu pesa za matumizi ya
nyumbani” alisema
Mize Hamad Sadiki, ni
miongoni mwa wapiga mbizi alisema kwasasa ana uwezo mzuri wa kuogelea lakini
anautumia uwezo huo kwenye shughuli zake za upandaji wa mwani pekee kutokana na
kukosekana kwa mashindano, matamasha na mabonanza ya mchezo wa kuogelea kwa
wanawake.
“Mimi ni Mama wa Watoto sita pia ni mjane nina uwezo mzuri wa kuogelea lakini nashindwa kupata faida ya mchezo huu kwasababu hakuna mashindano ya mara kwa mara na badala yake natumia uwezo huu katika shughuli zangu za mwani tu” alisema
Fatma Hamd Ali, mwanamke mwenye umri wa miaka 23, mwenye shauku na kipaji kizuri cha kuogelea anawaomba wadau wa michezo kuandaa mabonanza na matamasha ya mashindano ya kuogelea ili waweze kuonesha vipaji vyao na kujipatia kipato.
Hamad Amini Ali ni Mratibu
wa Kamisheni ya Utalii Pemba, alisema kuna kila haja ya kuwashirikisha wanawake
wenye uwezo wa kuogelea kwenye Matamasha na Mabonanza ya Utalii wanayoyafanya
ili kuboresha uwezo wao na kujipatia kipato
Alisema “Sisi kama kamisheni ya Utalii tumelipokea kwa mikono miwili ombi la akina mama hao na tutaenda kuwatembelea ili kuwafahamu lakini mwezi Novemba mwaka huu tutakuwa na Bonanza la Utalii Kisiwani Pemba tutaanda mashindano maalumu ya kuogelea kwa wanawake ili nao waweze kushiriki katika mashindano hayo”
Wadau na wananchi mbali
mbali Kisiwani Pemba wanashauku ya hali ya juu kuona mashindano ya kuogelea ya
wanawake kwani muda mrefu wanashuhudia mashindano hayo kwa jinsia ya kiume
pekee.
Shamimu Omar Shake Mkaazi
wa Tibirinzi Chake Chake alisema “Watu wengi wanadhani mwanamke hana uwezo
mzuri wa kuogelea kama mwanaume kwahivyo ikitokea kuna wanawake wanaogelea
vizuri kama wanaume hilo litakuwa ni jambo jema na kuvutia sana na wanawake
wengi watahamasika kuingia kwenye mchezo huo pamoja na kushiriki katika
mashindano mbali mbali”
Asha Ussi Makame ni mkaazi
wa Ndagoni, alisema wanajamii walio wengi wengi hawa Imani na wanawake katika
mchezo huo hivyo kuwepo kwa wanawake ambao wanafanya vizuri katika mchezo
kutasaidia kuondosha Imani potofu kwa baadhi ya wanaume kutokana na Imani hiyo
potofu kwa wanawake
“wanaume wengi hawana Imani na sisi wanawake kwenye mambo mbali mbali ikiwemo michezo, uongozi nakadhalika wanatuona kama viumbe lege lege tusioweza lolote zaidi ya majukumu ya nyumbani kwahivyo kuwepo kwa wanawake kama hao wenye uwezo mzuri wa kuogelea kutapelekea wanaume kuondokana na dhana hizo mbaya kwetu lakini pia itawahamasisha wanawake wengine kuingia kwenye mchezo huo” alisema





Comments
Post a Comment