“Waandishi zijueni Sheria za habari zenye mapungufu muongeze nguvu kuzitetea ili zifanyiwe mabadiliko” Dc Mjaja
Hassan Msellem.
Waandishi wa habari Kisiwani Pemba
wametakiwa kuzifahamu Sera na Sheria za habari zilizopitwa na wakati ili
kuongeza nguvu katika utetezi na kufanyiwa marekebisho chanya.
Mapema akifungua mafunzo ya siku moja
kwa waandishi wa habari Kisiwani Pemba Mkuu wa Wilaya ya Mkoani Khatibu Juma
Mjaja, amesema waandishi wa habari ni wadau wakubwa wanaoweza kuleta mabadiliko
ya Sheria za habari ambazo zinaonekana kukinzaba na uhuru wa habari na
Wanahabari.
Aidha mkuu huyo amewaomba waandishi
hao kuzifahamu Sheria za mitandao ya kijamii pamoja na takwimu ili kuandika
habari zenye ukweli na kuleta mabadiliko chanya kwa jamii.
“Kwahivyo wajibu wetu wanahabari nikuzifahamu
sheria za habari mbali mbali wengi wetu tunafanyakazi na online media
tunafanyakazi za takwimu, kwahivyo ni wajibu wetu kuzifahamu hizo sheria ili
tufanye kazi zetu kwa ufanisi” alisema
Kwa upande wake Katibu Mtendaji kutoka Baraza la Habari Tanzania (MCT) Kajubi
Mukajanga, amesema ili kuchochea nguvu ya marekebisho na maboresho ya Sheria
kandamizi za uhuru wa habari wanahabari hawana budi kuzifahamu Sheria hizo.
“Ni lazima wanahabari wazielewe
sheria hizo kwasababu kuna usemi kwamba kutojua sheria sio utetezi pale
unapoivunja walau wajue vifungu ambavyo vitawahusu mara Kwa mara” alitoa
ushauri
Nae wakili kutoka Baraza la Habari
Tanzania Mpale Mpoki, amesema ibara ya 18 ya katiba ya jamhuri ya Muungano ya
Tanzania na ile ya Zanzibar imeruhusu uhuru wa kutoa maoni, hivyo basi amesema
uhuru wa kutoa maoni ni haki ya msingi ya mwanadamu licha uhuru huo kuminywa
kwa baadhi ya wakati.
“Uhuru
wa maoni ni kitu cha msingi katika maendeleo na kutafuta ukweli na katika
kuimarisha demokrasia na utawala bora” alieleza
Shifaa Said Hassan ni Afisa
program mwandamizi wa baraza la habari Tanzania upande wa Zanzibar, amesema
Sheria ya mwaka 1988 ya wakala wa habari na magazeti ni Sheria inayokandamiza
uhuru wa habari, hivyo basi amewataka waandishi hao kuendelea kufanya
uchechemuzi katika kazi zao ili kuhakikisha mabadiliko katika sheria hizo
yanafanyika.
“Kwahivyo tukingalia tutaona kuwa sheria
zimetungwa muda mrefu sana na haziendani tena na mazingira ya sasa katika
tasnia ya habari kwahivyo wanahabari ni jukumu letu kuhakikisha tunashirikiana
kuandika habari na kufanya vipindi ambavyo vitachochea kufanyiwa marekebisho
chanya” alisema
Ameongeza kuwa bado kuna uminywaji
mkubwa wa uhuru wa habari nchini kwa waandishi kutokuwa na uhuru wa kufanya
kazi zao ipaswavyo ikiwemo kunyimwa taarifa, kupewa vitosho, kupigwa, kutekwa,
kunyanyaswa kudhalilishwa pamoja kufungwa kwa vyombo vya habari.
“Kama tunavyofahamu mara kwa mara tunapata taarifa za vyombo vya habari mbali mbali kufungiwa na baadhi ya wanahabari kupigwa na kudhalilishwa hii yote inatoa picha kuwa bado uhuru wa vyombo vya habari na wanahabari hatujakuwa na uhuru wa kuridhisha katika utekelezaji wa majukumu yetu” aliongeza
Akitoa ufafanuzi juu ya tuzo zinazotelewa na baraza hilo Afisa programu kutoka
baraza la habari Tanzania (MCT) Saumu Mwalimu, amewaomba wanahabari hao
kuandika habari zinazogusa maisha ya wananchi nakuleta mabadiliko chanya katika
jamii ili ziweze kuwa na vigezo vya kuchaguliwa kuwania tuzo hizo
“Kama tunavyojua kwamba baraza la habari Tanzania kila mwaka hua tuna mashindano ya kuwania tuzo katika categories mbali mbali hivyo basi niwasihi mufanye kazi zenye kuleta mabadiliko Fulani katika jamii na sio kuandika habari nani kasema ambazo hazimgusi mwananchi wa kawaida” alieleza afisa programu
Essau Kalikubira ni mwandishi wa UGA
ONLINE TV, amesema sheria ya usimamizi wa vyombo vya habari vya mtandaoni ni
sheria kandamizi kwani inanyima uhuru wa waandishi kuafanyakazi ipaswavyo,
hivyo basi ameliomba baraza la habari Tanzania kuendelea kukutana na wadau wa
Sheria ili kuifanyia marekebisho Sheria hiyo.
“Kwakweli
hii Sheria ya Mitandaoni bado naiyona ni Sheria kandamizi sana kwa waandishi wa
habari wa mtandaoni kwasababu inamfanya mwandishi ashindwe kufanyakazi kwa
ulaini na haraka kwani kila tukio inamlazimu kutoa taarifa kwa mamlaka husika
ndipo aweze kufanyakazi” alisema
Nao waandishi hao wameahidi
kuyafanyia kazi mafunzo hayo na kuwa mabalozi wazuri kwenye vyombo vyao ili
kuhakikisha wanafanyakazi kwakuzingatia Sheria pamoja na kuongeza nguvu katika
uchechemuzi wa marekebisho ya Sheria hizo.
Waandishi wa Habari Pemba wakiwa katika mafunzo ya siku moja ya kuwajengea uwezo Waandishi wa Habari kuhusu Sheria mbali mbali za Habari.
Bado Waandishi wa habari nchini
Tanzania wanatumia Sheria kuu za habari ambazo ni Sheria Nambari 5, ya mwaka
1998 ya usajili mawakala wa habari, magazeti na vitabu na Sheria ya tume ya
utangazaji Zanzibar nambari 7 ya mwaka 1997 ambazo zinaonekana kuminya uhuru wa
Habari na wanahabari
Mwaka 2021, vyombo kadhaa vya Habari
kama vile magazeti na runinga vilifungwa kwa nyakati tofauti pamoja na baadhi
ya wandishi kunyanyaswa na kupigwa.
Miongoni mwa vyombo hivyo ni gazeti
la Raia Mwema ambalo lilifungiwa kwa kipindi Cha Siku 30, gazeti la Uhuru siku
14, Wasafi TV miezi 6, kufungiwa Kwa Kipindi Cha Take One Cha Clouds TV kwa
kipindi cha miezi 3 pamoja na kupigwa kwa mwandishi wa Habari wa gazeti la
Mwananchi Zanzibar Josse Mikofu.
Mafunzo hayo ya Siku Moja
yaliyojumuisha Wanahabari kutoka vyombo mbali mbali Kisiwani Pemba yameandaliwa
na Baraza la Habari Tanzania (MCT).
Afisa Habari kutoka Chama Cha
Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) Kisiwani Pemba Gaspery Charles,
akieleza jinsi alivyowahi kushiri katika tuzo za EJAT nakuibuka mshindi.




Comments
Post a Comment