Habari Na, Hassan Msellem, Pemba.
Waandishi Kisiwani Pemba watakiwa kufuata maadili ya kazi zao, ili kuepuka kuingia kwenye makosa pamoja na kuandika habari zitakazoweza kutoa mchango kwa taifa.
Akizungumza na waandishi wa habari katika mkutano wa maadhimisho ya siku ya uhuru wa habari, leo Mei 18, 2024 uliofanyika ukumbi wa Chuo cha Samail Gombani Chake chake Pemba, Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba Mattar Zahor Massoud, alisema Waandishi ni sauti ya wasio na sauti hivyo wanapaswa kuandika habari ambazo zitaweza kuwasaidia Wananchi.
Aidha amewataka Waandishi hao kufuata maadili na ufanisi katika kazi zao Ili kuepukana na makosa mbali mbali pamoja na kuandika habari zenye kuleta mabadiliko chanya katika Umma.
"Siku hii ya uhuru wa habari ni muhimu kujitafakari kwamba tunafanya kazi kwa kiasi gani, tuna uhuru kiasi gani, vikwazo gani tunavyopitia na kupanga mikakati ya kuweza kutatua," alisema Mkuu huyo.
Mkuu huyo aliwataka waandishi hao kuibua changamoto za wananchi na kuzisemea, ili ziweze kupatiwa ufumbuzi, kwani sauti ya mwandishi ndio inayosaidia katika kuleta mabadiliko na maendeleo katika nchi.
Aidha aliwataka waandishi kuelimisha jamii juu ya kuhifadhi mazingira, ili yawe safi na kuweza kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ambayo yamekuwa yakiathiri maisha ya wananchi.
Kwa upande wake Afisa Mdhamini Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Pemba Mfamau Lali Mfamau, aliwasisitiza Waandishi hao kuwa na kadi maalumu zinavyotolewa na idara ya Habari maelezo Ili kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi sambamba na kuwataka Waandishi wanaomiliki runinga za mtandaoni kuvisajili vyombo vyao Ili viweze kutambuliwa na kufanya kazi kwa kufuata maadili ya Habari.
"Niwaombe waandishi wote wawe na vitambulisho maalumu vinavyotolewa na idara ya Habari maelezo Ili muwe huru katika utekelezaji wa majukumu yenu napia niwaombe wale wote wenye online TV na blogi wajisajili na kutafuta kadi ya uandishi, kwani kuna baadhi ya watu wanatumia mwamvuli wa waandishi kujifanya mwandishi na kuleta taharuki kwa Umma," alisema Mdhamini huyo.
"Tena inasikitisha sana kuona baadhi ya viongozi wa chama na Serikali wanatafuta watu ambao hawana taaluma ya habari na kuwatumia kama Wana habari mbona hawajifanyi madaktari, askari au wanajeshi kwanini mtu ajifanye mwandishi wa Habari haliyakuwa hana taaluma ya habari kwakweli nachukizwa sana na hii tabia na naahidi Mimi kama afisa mwenye jukumu la kusimamia tasnia ya Habari Kisiwani Pemba nitahakikisha nawachukulia hatua za kisheria wale wote ambao wanajifanya Waandishi wa Habari ambao hawana taaluma ya habari" alisema
Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Pemba (PPC) Bakar Mussa Juma, alisema waandishi wa habari katika Klabu hiyo wanafanya kazi vizuri na kuzingatia maadili ya uandishi wa habari, hivyo ameiomba jamii na viongozi mbali mbali kuendelea kuwapa ushirikiano ili waweze kutekeleza majukumu ya kazi zao kwa uhuru na ufanisi zaidi.
Aliongeza kuwa Klabu ya Waandishi wa Habari Pemba ina malengo ya kuanzisha Radio na television ili kutoa fursa kwa Waandishi wa Habari kufanya kazi zao ambapo kwa sasa wameanza na blogi ambayo imeanza kutoa mafanikio makubwa kwa Klabu hiyo.
Akiwasilisha mada katika maadhimisho hayo mwandishi wa habari na Mjumbe kutoka PPC Bwana Gasper Charles, alisema waandishi wa habari wana jukumu la kulinda na kuelimisha jamii kuhifadhi mazingira ambayo yanayopelekea athari za mabadiliko ya tabia ya Nchi ambayo yamekuwa ni tatizo linalopaswa kupigiwa kelele mara kwa mara.
Maadhimisho hayo ya siku ya uhuru wa habari yamefanyika katika Ukumbi wa Samael Gombani Chake Chake ambayo yameandaliwa Klabu ya Waandishi wa Habari Pemba (PPC) kwa ufadhili wa Umoja wa Vilabu vya Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC).

Comments
Post a Comment