Na, Hassan Msellem, Pemba
Mwandishi mwandamizi Zanzibar Bi. Hawra Shamte, amesema katika miaka ya hivi karibuni michezo imedhihirisha uwezo wake mkubwa wa kuendeleza uwezeshaji wa Wanawake na wasichana, hivyo jamii inapaswa kubadili mitazamo hasi juu ya suala la michezo kwa Wanawake ili nao waweze kupata haki yao ya msingi ya kushiriki katika Michezo.
Ameongeza kuwa michezo huchukuliwa kuwa ni haki ya wanaume pekee ambapo dhana hiyo hupelekea wavulana kutilia maanani zaidi suala la michezo na wasichana wakijikuta wanaachwa nyuma na kupelekea kutokuwepo kwa usawa wa Kijinsia kwenye michezo.
Sambamba na hilo amesema michezo inahamasisha kuzungumza na Vijana na kuunganisha vizazi kijamii na kiutamaduni, hivyo Waandishi wa Habari na wadau wa michezo wana jukumu la kuihamaisha jamii kuwa na mitazamo mizuri juu ya usawa wa Kijinsia katika Michezo.
"Linapokuja suala michezo kuanzia ngazi ya jamii Hadi taifa linaonekana ni jambo linalowahusu wavulana peke yake, kiasi kwamba wasichana wamejikuta wao hawahusiki kabisa kwenye michezo Hali hii inapelekea usawa wa Kijinsia kwenye michezo kubaki kuwa ndoto tu, hivyo ni wajibu wenu Waandishi wa Habari kuanza kuandika habari zinashajihisha na kuonesha umuhimu wa usawa Kijinsia kwenye michezo katika jamii zetu" alisema
Alisema licha ya wavulana kuona wao ndio pekee Wana haki ya kushiriki katika Michezo bado Kuna tatizo la unyanyapaaji wa Kijinsia kwani wanaume ambao wanaonekana kutokuwa na uwezo mzuri wa kushiriki kwenye michezo hubaguliwa na wanaume wenzao na kujiona wamekosa dhaifu na wamekosa thamani jambo ambalo hupelekea baadhi yao kujiingiza kwenye vitendo viovu ikiwemo vya utumiaji wa dawa za kulevya na kushiriki mapenzi ya jinsia moja.
Alisema "Hii dhana potofu haiwaathiri wasichana tu, Bali hata wavulana ambao walitegemewa kuwa wakakamavu, wavulana ambao hawana uwezo wa ukakamavu wa kimwili au Wana michezo wazuri hupata dhihaka na aibu kulingana na itikadi Kali ya kiume inayojumuisha nguvu, misuli, ukosefu wa huruma"
Amenena hayo katika Ofisi za Chama cha Waandishi wa Habari Tanzania Mkanjuni Pemba katika mafunzo ya siku tano kwa Waandishi wa Habari Kisiwani Pemba, katika mradi wa mwaka mmoja katika kukuza usawa wa Kijinsia katika Michezo (Cohort Gender and Sports) ambao umeanza Mwezi March 2024 na kutarajiwa kukamilika February 2025.

Comments
Post a Comment