Skip to main content

Sheria dhaifu za habari, kikwazo cha Maendeleo Zanzibar.

 Na, Hassan Msellem


MOJA ya sheria kongwe na inayotajwa kutokwenda sambamba na uhuru wa vyombo vya habari, ni ile nambari 5 ya mwaka 1988 ya Magazeti, Vitabu na Mawakala wa Habari Zanzibar.

 

Ni miaka 34 sasa, sheria hii inaendelea kutumika Zanzibar, na kutajwa kuathiri na kutishia utendaji kazi wawaandishi wa habari visiwani.

HISTORIA.

Sheria hiyo tokea mwaka 2010, ilianza harakati za kutaka kufutwa, kwa wadau wa habari kujikusanya pamoja, ili sasa iwe na sheria moya ya habari.

 

Kwa wakati huo, tasisi za Baraza la Habari Tanzania ‘MCT’ –ofisi ya Zanzibar, vyama vya waandishi wa habari, taasisi za haki za binadamu na wizara husika, zilianza harakati hizo.

 

Mara kadhaa, kulikuwa na taarifa kuwa, mwaka ujao au mwakani Zanzibar itapatikana sheria mpya ya habari, ambayo itakuja kufuta sheria ya Magazeti nambari 5 ya mwaka 1988 na ile ya Tume ya Utangaazji nambari 7 ya mwaka 1977.

 

Ilikuchakua takriban miongo miwili, kupita bila Zanzibar kuwa na sheria mpya, ingawa kwa Tanzania bara, wao walifanikiwa kufuta sheria ya Magazeti ya mwaka 1976, na kuwa na sheria ya Huduma ya vyombo vya habari ‘MSA’ ya mwaka 2016.

Kwa miongo miwili, wadau wa habari juhudi zao za kuwa na sheria mpya ya habari ziligonga ukuta, na harakati hizo zikaanza tena miaka ya 2018/2019.

SABABU ZA WADAU KUFUTWA KWA SHERIA YA MAGAZETI, VITABU NA MAWAKALA WA HABARI NO 5, 1988.


Sheria hii yenye vifungu 81 na sehem 10, sasa inatimiza miaka 34, tokea kutungwa kwake, na kwa maana nyingine, vipo vifungu zaidi ya 40, ambavyo vyengine vinahitaji kufutwa.


Vifungu vyengine vikihitajika kufanyiwa marekebisho na vyengine, vilivyobeba maneno makali kama uwezo wa waziri, waandishi kudhibitiwa na kufanya uchochezi.


Kwenye sheria hii, ambayo kwa sasa Chama cha Waandishi wa habari Wanawake Tanzania TAMWA-Zanzibar kwa ufadhili wa Internews, wanaharakishwa kufutwa kwa sheria hiyo.


VIFUNGU KANDAMIZI KWA UHURU WA HABARI.


Moja ya kifungu ambacho, kwa sasa wadau wanataka kifutwe ni kile cha 43, ambacho chenyewe, kinaeleza ‘uwezo wa ofisa aliyeidhinishwa’.


Ambapo kwa mujibu wa sheria hiyo, ofisa aliyeidhinishwa ni Polisi mwenye cheo cha Msaidizi Ofisa Mkaguzi au mwenye cheo cha juu ya hapo.


Mchambuzi wa sheria za habari Zanzibar Hawra Shamte, anasema, kwa sasa sheria hiyo na hasa kifungu cha 43 wanakiona, hakina mantiki.

‘’Makosa yote yanayotokana na waandishi wa habari yana sura ya madai na sio jinai, sasa iko wapi nafasi ya Polisi kuingia, kupekua kwenye vyombo vya habari,’’anahoji.


‘’Mfano kifungu (2) (a) kinaeleza uwezo wa ofisi huyo kuwa ‘anaweza kuingia sehemu yoyote, jengo, chombo cha ardhini, angani ambamo anaamini kwa maoni kuwa, mna vifaa vya habari, vilivyopangwa au vitakavyopangwa kukusanyia habari,’’   

 

Hata kifungu kidogo cha 2 (b) kikaongeza kuwa, ofisi huyo anaweza ‘kuchunguza mchakato wowote ambao unaonekana kuelekea kukusanya au kutoa habari yoyote ’.

 

Kubwa zaidi ambalo ni ukiukwaji wa uhuru wa habari, kifungu cha (c) kinampa uwezo ofisi hiyo ‘kumtaka mwandishi wa habari yeyote, kutoa vitendea kazi vyake, gazeti au waraka ambao, uko chini yake kukabdhi kwake’.


Kifungu 2 (d) ofisi huyo amepewa mamlaka ya ‘kunakili sehemu yoyote ya vitendea kazi vya waandishi wa habari au akiamiani tu kufanya hivyo, kuna uhusiano na uchunguuzi wake juu ya kosa chini ya sheria hii’.


Kubwa zaidi, pia ofisi hiyo kwenye kifungu hicho cha 43 (2) (e) anaweza ‘kuagiza taarifa zenye uhusiano na uchunguuzi wake kutoka kwa mtu yeyote, ambae anaamini aliajiriwa au ataajiriwa katika jengo alilokuwa akitunza kumbu kumbu’.


Pamoja na uwezo huo, ambao wadau wa haki za uhuru wa habari wanaona ni uminywaji wa haki za waandishi wa habari, sasa kifungu cha 44 kimekuja kumlinda.


Kifungu hicho 44 (1) kinaeleza kuwa, ‘mtu yeyote atakayempinga, kumzuia, au kumkwaza kwa ofisa huyo atakuwa ametenda kosa’


Na adhabu kwa kosa hilo lipo kifungu cha 73, ambapo ni faini ya shilingi 200,000 au kifungo cha miaka miwili chuo cha mafunzo au adhabu zote mbili kwa pamoja.


WADAU WA HABARI WANASEMAJE JUU YA KIFUNGU HIKI.

Kwa upande wake mwandishi wa habari mwandamizi Zanzibar Rashid Omar Kombo, amesema kifungu cha sheria kinachomruhusu afisa wa Polisi kuchunguza mchakato wowote au utendaji wa masuala ya habari kinyume na hati ya mahakama ni Sheria zinazokinzanza na mikataba mbali mbali ya kikanda na kimataifa juu ya uhuru wa vyombo vya habari.


“Kimsingi mataifa yote ya kidekrasia ambayo yanafuata misingi ya demokrasia na utawala bora masuala ya afisa wa polisi kukamata na kukagua yanahitaji idhini na vibali vya mahakama afisa wa Polisi hawezi kuwa yeye ndiye anatuhumu na yeye ndiye anakamata hiyo itakuwa ni Sheria ya ajabu” alisema


Fathiya Mussa Said ni mratibu wa chama cha waandishi wa habari wanawake Tanzania Kisiwani Pemba (TAMWA), amesema uwepo wa kifungu cha sheria kinachompa mamlaka afisa yoyote wa Polisi kufanya ukaguzi wa majengo pamoja na kukamata gazeti ni kifungu cha sheria ambacho inakandamiza uhuru wa vyombo vya habari na wanahabari kwa ujumla.


"Lakini sheria yetu ya Mgazeti nambari 5 ya mwaka 1988 ya Zanziba na hasa kifungu cha 43 kinaipinga hata katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, iliyotoa haki ya kutoa maoni,’’anaeleza

Nihifadhi Issa mwandishi wa Kati Fm Radio, anasema kifungu hicho sio rafiki, na hakitarajii kukiona kwenye sheria mpya ijayo ya habari.

Anasema "studio na vyumba vya habari ni ofisi nyeti kama zilivyonyengine, hivyo utaratibu wa kuingia, uwepo kama zilivyo ofisi nyingine" anahoji


Mwandishi wa UGA ONLINE TV Essau Simon Kalikubilla, anasema kifungu hicho hakifai kuwepo, maana kinahalalisha ukandamizaji wa uhuru wa waandishi wa habari.


Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Tanzania ‘MCT’ Kajubi Mukajanga wakati akizungumza na waandishi wa habari kisiwani Pemba wiki iliyopita, alisisitiza vyombo vya dola kuwaachia waandishi watekeleze kazi zao.


‘’Kuwapasha habari wananchi juu ya matukio ya ndani na nje ni haki kikatiba, sasa kama kuna sheria au kifungu kinampa uwezo mkubwa Polisi kuingia na kufanya atakavyo sio sahihi,’’anasema.


Mjumbe wa Kamati tendaji wa Jumuiya ya wanawake wenye ulemavu Zanzibar ‘JUWAZA’ Hidaya Mjaka Ali, anasema sheria bora ni chachu ya kupata waandishi wa habari bora.


Kamanda wa Polisi mkoa wa Kusini Pemba, anasema sio sahihi kwa afisa wa Jeshi la Polisi mwenye cheo chochote anaweza kuvamia ikiwa hakuna viashiria vya uhalifu.


Mwandishi wa blog ya The Chanzo Najat Omar, alisema sheria hiyo imeshapitwa na wakati na moja ya vifungu vibaya ni cha 43 na vifungu vyake vidogo.


‘Haiwezekani suala la haki ya kikatiba ya kupata na kutoa habari, apewe uwezo wa kupindukia Polisi, juu ya kuingia na kupekua kwenye ofisi za waandishi wa habari,’’alissema.


Mchambuzi wa sheria za Habari Zanzibar Hawra Shamte wakati akiwasilisha mada ya Sheria zenye mapungufu ndani ya ukumbi wa Tamwa, Pemba alisema kwenye nchi zinazojali kwa vitendo utawala bora na utawala wa sheria, suala la kupata na kutoa habari haliwekewi masharti mazito.


Mwenyekiti wa klabu ya waandishi wa habari Zanzibar ‘ZPC’ Abdalla Abudull-rahman Mfaume na mwenzake wa PPC Bakari Mussa Juma, walisema vifungu ambavyo vinampa wasi wasi waandishi wa Habari katika kutekeleza majukumu yake havipaswi kufumbiwa macho na badala yake mamlaka husika zinapaswa kusikiliza maoni ya wadau wa Habari na kuvifanyia marekebisho vifungu na sheria hizo.


Mhariri wa habari wa shirika la Magazeti ya serikali Zanzibar Haji Mwadini aliwahi kusema kuwa, ukuaji wa maendeleo ya taifa lolote duniani, waandishi wa habari mchango wao upo.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kusini Pemba Abdalla Hussein Mussa, alisema Sheria inayomruhusu afisa yeyote wa Jeshi la Polisi anaweza kukamata Gazeti lolote, popote linapopatikana haipo sahihi licha ya kwamba Jeshi la Polisi linajukumu la kusimamia usalama katika eneo husika, na kupendekeza Sheria hiyo ibadilishwe ifanyiwe marekebisho.


Hakimu wa Mahakama ya Mkoa Chake Chake Faraji Shomari Juma, alisema Sheria inayompa ruhusa hakimu kumpa hati inspekta wa Jeshi la Polisi ni sahihi kwani baadhi ya maudhui ya Habari yasipodhibitiwa yanaweza kupelekea athari kubwa.


NINI KIFANYIKE?

Kaimu Mratibu wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ‘ZLSC’ Pemba Safia Saleh Sultan, anasema lazima kwenye sheria ijayo ya habari, kifungu hicho kifutwe.


‘’Sheria ijayo ya habari, sitamani kurejeshwa kwa kifungu hichi, maana kwa upande mwengine ni kudhoofisha juhudi za waandishi katika kazi zao,’’anasema.


Mkuu wa wilaya ya Mkoani Khatib Juma Mjaja, anasema sheria bora ya habari huchangia kuwa na jamii bora na inayofanya uamuzi sahihi.


Zuhura Juma Said mwandishi wa habari wa Shirika la Magazeti Pemba, anasema sheria hiyo ya Magazeti, Vitabu na Mawakala wa Habari nambari 5 ya mwaka 1988, imekuwa kikwazo kwao.


Mwandishi wa habari Plus Fm Radio Khalfan Abdul-kadir, anasema sheria hiyo hasa kwenye upatikanaji wa kibali umekuwa shida.


Mkurugenzi wa TAMWA-Zanzibar Dk. Mzur Issa Ali, anasema ujio wa sheria mpya ya habari vifungu vinavyompa uwezo mkubwa waziri visiwmo.


‘’Ndio maana TAMWA -Zanzibar kwa kushirikiana na wafadhili wetu Shirika la Internews Tanzania tunaomradi wa miezi minne, ili kuwawezesha waandishi, kusukuma upatikanaji wa sheria mpya habari Zanzibar,’’anasema.

                               Mwisho.

Comments

Popular posts from this blog

MWANAMKE AJINYONGA, SABABU WASI WASI - PEMBA

NA, HASSAN MSELLEM - PEMBA PICHA KUTOKA MAKTABA Mwanamke aliyefahamika kwa jina la Raya Darusi Abdallla miaka 48, mkaazi wa Mbuzini Wilaya ya Chake Chake Mkoa wa Kusini Pemba, amefariki Dunia kwa kidaiwa kujinyonga kutokana na Msongo wa mawazo. Tukio Hilo limetokea Novemba 30.2025 saa 11 alfajiri huko Mbuzini Wilaya ya Chake Chake Mkoa wa Kusini Pemba. Omar Salum Ali, ambaye ni shemeji wa marehemu amesema kabla ya marehemu alikuwa na sumbuliwa na Msongo wa mawazo kutokana na kumpoteza kaka yake ambaye alifariki hivi karibuni, kugundulika kuwa ana maradhi ya sukari, mtoto wake wa kiume wa miaka 25, kuwa na ugonjwa akili hali iliyopelekea kupatwa na Msongo wa mawazo na kuamua kujinyonga. Katibu wa Sheha (Katibu wa Mwenyekiti) Shehia ya Mbuzini Yakub Ali Msabah, amesema alipata taarifa za tukio Hilo kutoka kwa Sheha wa Mbuzini kuhusu tukio baada ya kufika eneo la tukio waliukuta mwili wa Mama huyo ukiwa unanin'gia kwenye dari ya Nyumba ambayo alikuwa anaishi zamani. Kutoka tarehe 18 ...

Mariam Muhene – mfano wa kuigwa kwa wanawake kwenye ulingo wa siasa ni

MAKALA NA, HASSAN MSELLEM -PEMBA Tangu Tanzania iruhusu mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, Mariam Muhene alijiunga na chama cha Civic United Front (CUF) ambapo mwaka 1995, aligombea nafasi ubunge wa viti maalumu na kuvuka hatua zote ikiwemo kula kiapo mahkamani lakini hakufanikiwa kukikalia kiti hicho. “Mwaka 1995 niligombea ubunge wa viti maalum na nikapita kila kipengele mtu wa kwanza wilaya, taifa bodi ya uongozi, nikala kiapo mahkmanai lakini katika nafasi mbili zilizoletwa kwa kila mkoa Kusini na Kaskazini Pemba mimi sikubahatika” amesema  Safari yake ya kisiasa za upinzani iliendelea na mnamo mwaka 2000, aligombea nafasi ya ubunge wa kuchahguliwa kupitia chama cha Allience for Democratic Change (ADC) Jimbo la Chake Chake lakini kutokana na changamoto zilizojitokeza ikiwe mawakala wa Chama chake kutokuruhisiwa kuingia kwenye vya kupiga kura jambo ambalo amesema lilichangia kukosa nafasi hiyo. Kwasasa Mariam Mohammed Muhene anashika nafasi ya Kamishna wa ADC kanda ya Pemba, nafas...

WATOTO KUJINYONGA ZANZIBAR, UTAFITI WAHITAJIKA.

HABARI NA, HASSAN MSELLEM, PEMBA Picha kutoka mtandaoni Visa vya watoto kujinyonga vimeanza kuwatia khofu na mashaka wazazi na walezi katika Visiwa vya Unguja na Pemba. Mashaka na khofu hiyo imeibuka baada ya matukio mawili mfululizo ya watoto wawili mmoja akiwa umri wa miaka (5) na mwengine (9) kuripotiwa kufariki dunia kwa kujinyonga kati ya tarehe 7 na 9 mwezi huu wa kumi mwaka 2025 kupitia kipindi cha Mawio kinachorushwa na Shirika la Utangazaji Zanzibar ZBC kila siku kuanzia saa 12:40 asubuhi. Katika tukio la kwanza mnamo tarehe 7.10.2025 mwandishi Masanja Mabula aliripoti tukio la Fatma Omar Kidere mwenye umri wa miaka tisa (9) mkaazi wa Mtondoo Jeuri Makaangale Wilaya ya Micheweni Mkao wa Kaskazini Pemba, amekutwa amefariki dunia na mwili wake ukiwa unanin’ginia kwa kutumia mtandio Jirani wa marehemu aliyefahamika kwa jina la Khamis Ali, amesema amepata taarifa za tukio hilo akiwa kazini baada ya kupigiwa simu na mke wake kumpa taarifa za kutokea kwa tukio hilo na kuondoka kazin...