Habari Na, Ahmed Abdulla.
LICHA ya elimu inayitolewa kwa jamii juu ya ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi, lakini bado baadhi yao wanashindwa kujitokeza katika kuwania nafasi hizo kutokana na ukosefu wa huduma mbalimbali za kijamii.
Hayo yalibainishwa na wahamasishaji jamii (CBs) katika ripoti za mikutano ya kijamii na kupata muongozo wa wawezeshaji walizoziwasilisha katika kikao kilichofanyika katika ukumbi wa skuli ya Jangombe.
Walisema miongoni mwa huduma hizo zinazokosekana ambazo zinawafanya baadhi ya wanawake washindwe kugombea nafasi za uongozi ni pamoja na ukosefu wa maji safi na salama, vitambulisho vya mzanzibar, vyeti vya kuzaliwa, miundombinu ya barabara za ndani na mambo mengine.
Walisema hali hiyo inawasababisha wanawake hao kutumia muda mwingi kutafuta huduma hizo na kushindwa kwenda kujishurikisha katika harakati za uongozi na kujitafutia maendeleo mengine ya kuinua uchumi wao.
Mhamasishaji jamii kutoka wilaya ya kati Bahati Issa Suleiman alisema licha ya kutolewa elimu kwa jamii ipo haja ya kuvifikia vyama vya siasa ili kuwahamasisha wanawake kuweza kugombea nafasi za uongozi.
"Kama hatutoingia katika vyama vya siasa kuwahamasisha hatuwezi kuwapata wanawake wataoweza kuwania nafasi za uongozi na badala yake tutakuwa tunasema tu miitaani,"alisema.
Mhamasishaji jamii kutoka Wilaya ya magharibi 'A' Fransisca Camilius Clement, alisema licha ya kuhamasishwa wanawake kushiriki katika nafasi za uongo lakini bado asilimia kubwa ya wanawake uwezo wao kiuchumi mdogo.
Alisema kutokana na hali hiyo ni vyema kuwezeshwa kiuchumi, hasa kupitia asilimia ambazo zimetengwa kwa ajili yao kupatiwa ili waweze kuzitumia kwa ajili ya kujipatia maendeleo.
"Kuna asilimia kumi zilizotengwa na Halmashauri ambazo asilimia nne zimewekwa kwa ajili ya kuwezeshwa wanawake, fedha hizo hivi sasa zimehamishiwa wizara ya Uwezeshaji, asilimia kubwa ya wanawake hawazifahamu fedha izo njia ya kuzipata, hivyo kunaumuhimu wa kufatiliwa ili kuweza kuwasaidia,"alisema.
Abdulrahman Khatib Mohammed kutoka Wilaya ya magharibi 'A' alisema ushirikia wa viongozi wa majimbo mdogo kwa wananchi haliambayo inasababisha kuwepo kwa changamoto nyingi na kushindwa kupatikana ufumbuzi.
Alisema hali hiyo husababisha hata kuwatia dosari baadhi ya wananchi wengine ambao wataonesha nia ya kugombea katika nafasi hizo.
Meneja miradi wa Chama cha Waandishi wa Habari, Wanawake Tanzania (TAMWA, ZNZ), Ali Mohammed, alisema ripoti hiyo wameipokea na wanaenda kujiaandaa zaidi kwa kuandaa mikakati ambayo itaweza kuweka mazingira mazuri kwa makundi hayo.
Alisema lengo la kuwaweka wahamasishaji jamii ni baada ya kubaini kwamba kundi hilo bado linakabiliwa na changamoto nyingi haliambayo inawasababisha kutofikia malengo yao ya kuwa viongozi.
Mratibu wa mradi wa kuwawezesha wanawake kushika nafasi za uongozi, kutoka Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA), Khamis Ali Rashid, aliwataka wahamasishaji jamii kutokata tamaa na badala yake kuendelea kuhamasisha wanawake kujitokeza katika nafasi hizo, licha ya changamoto wananzokabiliana nazo.
Mkutano huo wa siku moja wa uwasilishaji ripoti za mikutano ya jamii umeandaliwa na ZAFELA kupitia mradi wa kuwawezesha wanawake kushiriki katika nafasi za uongozi (SWIL), unaotekelezwa kwa pamoja baina ya TAMWA ZNZ, ZAFELA na PEGAO chini ya ufadhili wa ubalozi wa Norway Tanzania.

Comments
Post a Comment